54
Sala ya kujikinga na maadui(Kwa Mwimbishaji: Na ala za nyuzi za muziki. Utenzi wa Daudi wakati mtu mmoja kutoka Zifu alipomwendea Shauli na kumjulisha kuwa Daudi amejificha kwao.) 1 Uniokoe, ee Mungu, kwa jina lako; unitetee kwa nguvu yako. 2 Uisikie, ee Mungu, sala yangu; uyategee sikio maneno ya kinywa changu. 3 Watu wenye kiburi wananishambulia; wakatili wanayawinda maisha yangu, watu ambao hawamjali Mungu. 4 Najua Mungu ni msaada wangu, Mwenyezi-Mungu hutegemeza maisha yangu. 5 Yeye atawaadhibu maadui zangu kwa uovu wao wenyewe; kwa uaminifu wako, ee Mungu, uwaangamize. 6 Nitakutolea tambiko kwa moyo mkunjufu; nitakushukuru kwa kuwa ni vema. 7 Maana umeniokoa katika taabu zangu zote, nami nimewaona maadui zangu wameshindwa.