36
Uovu wa binadamu(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Daudi, mtumishi wa Mwenyezi-Mungu) 1 Dhambi huongea na mtu mwovu, ndani kabisa moyoni mwake; jambo la kumcha Mungu halimo kabisa kwake. 2 Mwovu hujipendelea mwenyewe, hufikiri uovu wake hautagunduliwa na kulaaniwa. 3 Kila asemacho ni uovu na uongo; ameacha kutumia hekima na kutenda mema. 4 Alalapo huwaza kutenda maovu, hujiweka katika njia isiyo njema, wala haachani na uovu. Wema wa Mungu 5 Fadhili zako ee Mwenyezi-Mungu zaenea hata mbinguni; uaminifu wako wafika mawinguni. 6 Uadilifu wako ni kama milima mikubwa, hukumu zako ni kama vilindi vya bahari. Wewe, ee Mwenyezi-Mungu, wawalinda wanadamu na wanyama 7 Jinsi gani zilivyo bora fadhili zako! Wanadamu hukimbilia kivulini mwa mabawa yako. 8 Wawashibisha kwa utajiri wa nyumba yako; wawanywesha kutoka mto wa wema wako. 9 Wewe ndiwe asili ya uhai; kwa mwanga wako twaona mwanga. 10 Uendelee kuwafadhili wale wanaokutambua; uzidi kuwa mwema kwa wanyofu wa moyo. 11 Usikubali wenye majivuno wanivamie, wala watu waovu wanikimbize. 12 Kumbe watendao maovu wameanguka; wameangushwa chini, hawawezi kuinuka.