4
Kuomba msaada jioni(Kwa Mwimbishaji: Na ala za nyuzi za muziki. Zaburi ya Daudi) 1 Ee Mungu mtetezi wa haki yangu, unijibu niombapo. Nilipokuwa katika shida, wewe ulinisaidia; unionee huruma na kusikia sala yangu. 2 Jamani, mtaniharibia jina langu mpaka lini? Mpaka lini mtapenda upuuzi na kusema uongo? 3 Jueni kuwa Mwenyezi-Mungu amejiteulia mwaminifu wake. Mwenyezi-Mungu husikia kila ninapomwomba. 4 Tetemekeni kwa hofu na msitende dhambi; tafakarini vitandani mwenu na kunyamaza. 5 Toeni tambiko zilizo sawa, na kumtumainia Mwenyezi-Mungu. 6 Wengi husema: “Laiti tungepata tena fanaka! Utuangalie kwa wema, ee Mwenyezi-Mungu!” 7 Lakini mimi umenijalia furaha kubwa moyoni, kuliko ya hao walio na divai na ngano kwa wingi. 8 Nalala na kupata usingizi kwa amani; ee Mwenyezi-Mungu, wewe peke yako waniweka salama.